Search

Monday, March 28, 2016

Wenye tumbili wao walia na serikali..

No comments


Wenye tumbili wao walia na serikali



CHAMA cha Wasafirishaji wa Nyara Tanzania (TWEA) Kanda ya Kaskazini kimeiomba serikali kufanya uchunguzi wa kina na kuwaachia wanachama wao waliokamatwa mwishoni mwa wiki kwa tuhuma za kusafirisha tumbili hai 62 bila vibali huku wakieleza kuwa wapo tumbili wengine katika mabanda yao.
Miongoni mwa waliokamatwa ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Arusha Bird Traders na raia wawili wa Uholanzi waliokamatwa mwishoni mwa wiki kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) wilayani Hai mkoani Kilimanjaro wakituhumiwa kusafirisha tumbili hao.
Akizungumza na waandishi wa habari jana hapa, Mwenyekiti wa Twea Kanda ya Kaskazini, Othman Bhoki alisema kukamatwa kwa raia hao wawili KIA ambao ni Arten Vardanian (52) na Edward Vardanian (46) pamoja na Idd Misanya ambaye ni Mkurugenzi wa kampuni iliyotumika kukamata tumbili hao ya Arusha Bird Traders ni kuwarudisha nyuma wafanyabiashara ambao wana vibali halali vya kuvuna tumbili hao.
Alisema wasafirishaji wa tumbili hao ambao ni Kampuni ya Arusha Bird Traders wana vibali halali vya kufanya biashara hiyo kwa maelekezo ya tangazo la Wizara ya Maliasili na Utalii.
Alisema suala hilo ni vyema likachunguzwa kwa kina kwani kampuni hiyo imewasilisha kibali halali cha kusafirisha wanyama hao chenye namba 29655 (Cites) kilichotolewa Februari 24, mwaka huu ambacho kinamalizika muda wake Agosti 23, mwaka huu.
Alisema kibali hicho kimeruhusu tumbili 62 kusafirishwa kwenda nchini Armenia na kukamatwa kwao kunaleta mkanganyiko kwani kwa mujibu wa kibali cha kukamata wanyama hao, kinaonesha kuruhusu daraja namba 13 la kuruhusu gawiwo la tumbili kuuzwa nje ya nchi.
Alisema aina ya tumbili waliozuiwa wapo katika mgawo wa Taifa iliyoruhusu wauzwe tumbili 5,000 kwa mwaka na wafanyabiashara na gawiwo hilo kwa daraja tajwa lina tumbili aina mbili; Velvet Monkey na Blue Monkey (400).
Alisema katika mazingira hayo wanashindwa kuelewa ni vigezo gani alivyotumia Waziri wa Maliasiali na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe kuzuia wanyama hao kwenda nje ya nchi kwani daraja lililokatazwa kufanyiwa biashara ni la 14 ambalo linahusu wanyama wakubwa hasa wale wenye pembe na kwato.
Alisema kinachoshangaza zaidi wakati tumbili hao wakizuiwa kusafirishwa huku wakurugenzi wakishikiliwa na Polisi, wanachama hao wa TWEA Kanda ya Kaskazini bado wana tumbili katika mabanda yao wanaosubiri kusafirishwa nje ya nchi katika masoko mbalimbali barani Ulaya.
“Tunalaani kuitwa watoroshaji wa wanyama hawa wakati tuna vibali vinavyoturuhusu kusafirisha wanyama hawa tunaomba uchunguzi wa kina juu ya suala hili ili tujue hatma ya raia hao wanaoshikiliwa na polisi maana hapa kuna mkanganyiko na hatujui Waziri Maghembe amezuia kwa kibali gani ni hiki tulichonacho au la,” alisema.
Naye Katibu wa Twea, Said Gumbo alisema kwa hatua hiyo ya Wizara kuzuia wanyama hao, wafanyabiashara hao wamewekwa katika mazingira magumu kwani wanaofanya biashara hiyo ni raia wa Tanzania wanaotafuta riziki zao kwa kufuata sheria na taratibu za nchi.
Aliiomba Serikali kufanya uchunguzi wa haraka wa tukio hilo na kuwaachia wanachama hao wanaoshikiliwa. Mwishoni mwa wiki, vyombo vya ulinzi na usalama kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) viliwanasa wafanyabiashara wawili ndugu raia wa Uholanzi wakijaribu kusafirisha tumbili kwenda nchini Armenia.
Wanyama hao wakiwa kwenye makasha sita tofauti ya kuhifadhia walikuwa wasafirishwe kwa ndege maalumu ya mizigo yenye namba EW/364G iliyosajiliwa Belarus kupitia Kampuni ya Arusha Freight Limited ya hapa.
Mbali ya raia hao wa Uholanzi pia wanamshikilia Mtanzania, Misanya ambaye ni Mkurugenzi wa kampuni iliyotumika kukamata tumbili hao ya Arusha Bird Traders anayedaiwa kuwauzia wanyama hao.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Kamishna Msaidizi wa Polisi, Wilbroad Mutafungwa alithibitisha kukamatwa kwa raia hao na wamehifadhiwa Kituo cha Polisi KIA huku uchunguzi zaidi wa tukio hilo ukiendelea.

Wanasayansi wadai povu la chura ni tiba

No comments

Wanasayansi wadai povu la chura ni tiba


Povu la churaGLASGOW, UINGEREZA
WANASAYANSI nchini Uingereza wamesema povu linalotolewa na vyura wadogo kwa ajili ya kulinda mayai yao linaweza kuponya majeraha ya wagonjwa walioungua kwa moto.
Pia wanaamini kuwa povu hilo linaweza kukusanywa na kusaidia mchakato wa matibabu kama kizuizi baina ya bandeji na ngozi iliyoungua.
Watafiti kutika Chuo Kikuu cha Strathclyde wameanza utafiti juu ya povu hilo linalotolewa na vyura wadogo kutoka kwenye kisiwa cha Tungara, huko Trinidad.
Vyura hao hutoa povu la urefu wa sentimita 5 kulinda mayai yao dhidi ya magonjwa na hali ya hewa kwa wastani wa siku tano.
Povu hilo limetengenezwa kwa aina tano za protini.
Doctor Paul Hoskisson na wenzake wanasema wameweza kuzichunguza aina nne za protini zinazopatikana kwenye povu hilo na kuchanganya na dawa zao ili kuipata tiba husika.
Watafiti hao watawasilisha kazi yao katika mkutano wa mwaka wa kituo cha uratibu wa shughuli za utafiti wa viumbe hai -Microbiology Society- utakaofanyika Liverpool.

Askofu amwangukia Magufuli

No comments

Askofu amwangukia Magufuli


Pg 1
>> Viongozi wa dini wasisitiza upendo, umoja katika familia
NA MWANDISHI WA GAZETI LA MTANZANIA, DAR ES SALAAM
ASKOFU wa Kanisa la Anglikani nchini (KAT), Dayosisi ya Mount Kilimanjaro (DMK), Askofu Stanley Hotay, amesema kanisa halina majipu ya kutumbuliwa kwa kuwa linatoa huduma zinazoisaidia Serikali kupeleka maendeleo kwa Watanzania.
Kauli ya Askofu Hotay aliyoitoa mjini hapa jana wakati wa Ibada ya Ijumaa Kuu iliyofanyika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid imekuja wakati mwenendo wa uongozi wa Rais John Magufuli ni wa kutumbua majipu kutokana na kile alichokisema Februari, mwaka huu wakati akizungumza na wazee wa Dar es Salaam kuwa alikuta uozo mkubwa serikalini.
Akizungumza wakati wa kumkaribisha mgeni rasmi katika ibada hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Daud Ntibenda, Askofu Hotay alipongeza juhudi na kazi kubwa inayofanywa na Serikali ya Magufuli.
Askofu Hotay ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Umoja wa Kanisa la Arusha alisema kumekuwapo na taarifa
za waraka wa kuondolewa kwa misamaha ya kodi kwa kanisa hatua aliyosema kama itatekelezwa itarudisha nyuma
juhudi za kuisaidia Serikali katika kuwaletea wananchi maendeleo.
“Tunakuomba mkuu wa mkoa utusaidie kufikisha hili. Lakini pia liangaliwe vizuri sisi hatuna majipu kabisa.
Tunasaidiana na Serikali katika kutoa huduma za kijamii,” alisema Askofu Hotay.
Kwa upande wake, Ntibenda, aliwaomba viongozi wa kanisa kuisaidia Serikali kuhamasisha vijana kufanya
kazi.
“Rais Magufuli amenipa majukumu ya kuhakikisha watu wanafanya kazi hasa vijana badala ya kucheza mchezo wa pool.
Tabia hii ikiachwa itatengeneza Taifa la wavivu na walalamikaji,” alisema Ntibenda.
Alisema Serikali itaendeleza ushirikiano uliopo baina yake na taasisi za dini ikiwa ni pamoja na kuhakikisha watu
wake wanaendelea kuabudu kwa amani na utulivu.
Katika ibada hiyo, Ntibenda, alilazimika kutoa namba yake ya simu ambayo ni 0766030000 na 0754604003
baada ya kuwataka wananchi wasikubali kutoa rushwa katika maeneo ya huduma za kijamii.
“Nawaomba wananchi nipigieni simu pindi mnapoombwa rushwa katika huduma za kijamii na maeneo mengine.
Nisaidieni kupambana na vita hii,” alisema Ntibenda ambaye namba yake ilisomwa kwa wananchi na Askofu Hotay.
MAGUFULI
Kwa upande wake, Rais Magufuli, aliwashangaza waumini wa Kanisa la Mtakatifu Petro lililoko Oysterbay jijini Dar  es salaam baada ya kusimamisha msafara wake na kisha kusalimiana na walemavu.
Tukio hilo lilitokea jana katika lango la kutokea kanisani hapo ambako alikwenda kuhudhuria Ibada ya Ijumaa
Kuu.
Magufuli alifika kanisani hapo mapema na kusali pamoja na waumini wa kanisa hilo na ibada ilipoisha alipanda katika gari lake na kuondoka.
Wakati akiondoka alikuwa akiwapungia mkono waumini hao na alipofika langoni hapo ghafla msafara wake ulisimama na kisha kushuka ili kuwasalimia waumini hao jambo lililowafanya wengine kusogea
ili kujua kilichotokea.
Magufuli alishuka na kuwafuata walemavu waliokuwa wamekaa jirani na lango hilo la kutokea na kuzungumza
nao.
Ingawa mazungumzo hayo hayakusikika, kitendo cha kushuka na kuzungumza na walemavu hao kiliwafanya watu waliokuwapo jirani na eneo hilo kuvutiwa na alipomaliza alipanda tena katika gari yake na msafara huo kuondoka kuelekea Ikulu.
Awali, akizungumza katika mahubiri hayo, Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Petro, Stephano Kaombwe, aliwasihi
Watanzania kuwa na moyo wa upendo.
Huku akinukuu katika Biblia Takatifu katika injili ya Yohana, Kaombwe alisema inashangaza kwamba Mungu
aliupenda ulimwengu hata akamtoa mwanaye wa pekee Yesu Kristo kwa ajili ya wanadamu lakini wenyewe bado
wanachukiana.
“Wanadamu hatukuumbwa tuteseke, ukisoma katika kitabu cha Mwanzo utaona Mungu aliwaweka Adam na
Hawa kwenye bustani ili waishi vizuri, wastarehe lakini walitenda uasi,” alisema Kaombwe.
LOWASSA
Kwa upande wake, aliyekuwa mgombea urais wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) na
Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, aliyeshiriki ibada hiyo katika Kanisa la Azania Front Kanisa aliwatakia
Watanzania washerehekee Sikukuu ya Pasaka kwa amani lakini alikataa kuzungumzia ya Zanzibar.
“Suala la uchaguzi wa Zanzibar siwezi kulizungumzia kwa sasa labda hapo baadaye lakini kufanyika kwa uchaguzi
huo ninamtukuza Mungu,” alisema Lowassa baada ya ibada hiyo kumalizika.
Awali akizungumza katika ibada hiyo, Mchugaji wa Usharika wa Azania Front, Charles Mzinga, alisema ni vyema wazazi watekeleze wajibu wao katika kuhakikisha watoto wanapata malezi bora.
“Watoto wetu tunapaswa kuwalea katika maadili yanayompendeza Mungu,” alisema mchungaji huyo.
Alisema kila mtu anapaswa kuwajibika ipasavyo ili kuhakikisha kila analolifanya linamtukuza Mungu ikiwa kazini
au katika jamii.
Wakati huohuo, katika mahubiri yake aliyoyatoa Kanisa Kuu Katoliki la Mtakatifu Joseph, Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Padre Nicholas Masamba, aliwataka Wakristo kuwajibika kutekeleza majukumu yao katika familia zao
na si kuwachia walimu peke yao.
“Tafakari hii ya kifo cha Yesu kusema yametimia, inarudisha swali kwetu ikitutaka tujiulize kuwa ni mangapi tumeyatimiza na sisi kwenye ngazi mbalimbali ikiwamo kazini, malezi ya familia na kwenye nafasi mbalimbali kama Wakristo,” alisema Padri Masamba.
Katika ibaada hiyo iliyohudhuriwa na waumini wengi akiwamo aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano
wa Kimataifa, Bernard Membe, alisema Wakristo wengi wamekuwa wakishindwa kutimiza majukumu yao katika
nafasi mbalimbali.
Habari hii imeandikwa na Faraja Masinde, Ruth Mnkeni na Veronica Romwald (Dar es Salaam) na Eliya Mbonea (Arusha)

KUTOKA  GAZETI LA MTANZANIA

Kwa nini tumbili, mijusi ni ‘dili’ Ulaya

No comments


Mjusi aina ya Agama
Mjusi aina ya Agama 


Mjusi aina ya Agama




Dar/Moshi.Siri ya utoroshaji wa wanyama na wadudu hai kutoka Tanzania kwenda nje ya nchi imebainika. Wamekuwa wakitumika katika nchi mbalimbali kwenye utafiti, mapambo na kitoweo.

Uchunguzi uliofanywa na waandishi wetu, umebaini matumizi hayo na kuwa wanyama wanaotakiwa kwa wingi ni mijusi ya bluu, kenge na tumbili wanaopelekwa katika nchi za Ulaya kupitia viwanja viwili vya ndege hapa nchini.
Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori, Herman Keraryo alisema mbali na wanyama hao, wengine wanaopelekwa nje ni jamii ya nyani, wadudu na ndege.
Alisema hakuna nchi ambayo imejitambulisha kipeke kununua wanyama hao, bali imekuwa ni biashara kati ya mzawa na mnunuzi.
Alipoulizwa kuhusu uhalali wa biashara hiyo, Keraryo alisema mfanyabiashara lazima awe na leseni inayotambuliwa na Serikali; “... na siyo kila ndege anasafirishwa au nyani, kuna aina ya ndege wasioruhusiwa ila kwa kutozingatia sheria, baadhi ya watu wanaivunja.” Mkurugenzi Mkuu wa zamani wa Tanapa, Gerald Bigurube alisema wanyama kama kobe na kakakuona nao wamekuwa wakisafirishwa zaidi kwenda Vietinam na China kwa matumizi ya chakula na dawa.
Alisema matumizi mengine ya wanyama hao wanaopelekwa Marekani na Ulaya yamekuwa ni kwa ajili ya shughuli za mapambo.
“Wanyama hai na wadudu kwa kifupi wana soko pana sana duniani na matumizi yake ni kama hayo lakini inakuwa vigumu kujua moja kwa moja wanapelekwa nchi gani,” alisema.
Bigurube alisema wanyama wengine wamekuwa wakipelekwa kwenye maeneo ya mafunzo ili watu wengine duniani wajifunze historia yao. Imeelezwa kuwa mijusi ya bluu ambayo inapatikana Tanzania pekee ndiyo inayotafutwa zaidi na kila mmoja umekuwa ukiuzwa kwa Euro 5,000 (Sh12.2 milioni.)
Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali ndani ya Idara ya Wanyamapori, wimbi la ukamataji na utoroshaji wa mijusi hiyo na tumbili linatokana na kuhitajika katika nchi mbalimbali kwa ajili ya utafiti.
“Kitu kinachoibwa zaidi sasa hivi nchini ni hao tumbili kwa sababu wanatumika sana huko nje kwa ajili ya utafiti wa kitabibu,” kilidokeza chanzo chetu na kuongeza: “Hata unavyoona, faru wanauawa ni kwamba wenzetu huko nchi za Asia wanaamini unga wake unasaidia kuongeza nguvu za kiume.”
Matumizi hayo yamebainika siku chache baada ya vyombo vya dola kuwashikilia raia wawili wa Uholanzi kwa kosa la kusafirisha tumbili 61 ambao walikuwa wapelekwe Albania kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (Kia).
Habari zilizopatikana juzi zilidai kwamba mmoja wa maofisa wanyamapori alipewa bakshishi ya Dola 3,000 za Marekani, sawa na Sh6.4 milioni za Tanzania katika ‘dili’ hiyo ya tumbili 61.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe alikiri kuwa tumbili na mijusi hao wa bluu ndiyo wanaowindwa zaidi kwa sasa; “... na huyo Williams Blue Lizard ni mjusi anayepatikana Kimboza na Ruvu. Ndiyo maeneo pekee duniani. Huyo mjusi anakaa juu ya miti kwa hiyo wanachofanya ni kukata mti na kuuangusha ndipo wanawakamata na kuwaweka kwenye mabegi. Wanafanya uharibifu mkubwa.”
Profesa Maghembe alisema mijusi hao huuzwa kati ya Euro 5,000 hadi 6,000 kila mmoja katika nchi za Ulaya.
Kuhusu tumbili, Profesa Maghembe alisema mpango ulikuwa ni kukamata tumbili 441 kwa awamu lakini kikwazo kikubwa kilikuwa ni upatikanaji wa kibali cha kuwasafirisha kwenda nje.
Alipoulizwa kwa nini raia hao wa Uholanzi wamekamatwa wakati walikuwa na kibali, alisema kibali hicho kilitolewa katika mazingira ya rushwa.
“Ni kweli walikuwa na kibali lakini kilitolewaje wakati nilishazuia na waraka ukatolewa? Lakini ujue hawakuwa na kibali pia cha kuwakamata hao wanyama,” alisema.
“Hili jambo lina njama kubwa na ndiyo maana tumeamua lichunguzwe na kile kikosi kazi cha kitaifa ambacho huchunguza makosa makubwa ya kihalifu,” alisisitiza.


Kutoka katika gazeti la

Mwananchi

hot weekly news

toniking wed designer

toniking wed designer